Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Hafla hizo zilizo fanyika maeneo mbali mbali nchini humo ziliambatana na maneno ya pole, mawaidha ya kidini na dua za kumuombea rehema na daraja ya juu Shahidi Kiongozi wa Mapinduzi ya Iran, Ayatollah Sayyed Ali Khamenei (ra), huku washiriki wakikumbuka mchango wake mkubwa katika kusimamia misingi ya haki, uadilifu na mapambano dhidi ya dhulma.
Kilichovutia zaidi katika mikusanyiko hiyo ni wigo mpana wa washiriki wake. Kwani, Sio Waislamu wa Kishia pekee waliojitokeza, bali pia Waislamu kutoka madhehebu mbalimbali pamoja na baadhi ya watu wasiokuwa Waislamu walihudhuria, wakionesha mshikamano wa kibinadamu katika kipindi hiki cha huzuni na maombolezo.
Washiriki walisisitiza kuwa; urithi wa fikra, msimamo na uongozi wa Ayatollah Khamenei (ra) utaendelea kuishi katika mioyo ya wapenzi wa haki na uhuru duniani, huku wakimuombea Mwenyezi Mungu amrehemu na amjaalie makazi mema Peponi.
Miongoni mwa taasisi zilizoandaa na kuratibu mahafali hayo ya maombolezo ni pamoja na Jumuiya ya Shia Ithnaasharia Tanzania (TIC), Kituo cha Jaamiatul Mustafa Tanzania, Taasisi ya Bilal Muslim Mission, Kituo cha Utamaduni cha Iran nchini Tanzania, pamoja na taasisi nyingine kadhaa za kidini na kijamii.
Katika nyoyo za wengi waliohudhuria, maombolezo hayo hayakuwa tu tukio la huzuni, bali pia yalikuwa ni ishara ya umoja, upendo na mshikamano kwa wanadamu katika kukumbuka maisha na harakati za kiongozi aliyegusa nafsi za wengi duniani.
















Maoni yako