Kwa mijibu wa Shirika la Habari la Hawza, Katika ziara hiyo, Sheikh Abubakar Zubeir na viongozi wenzake waliongozana na mwenyeji wao wa Mkoa wa Dar es Salaam, Kaimu Sheikh wa Mkoa, Sheikh Abbas bin Sheikh Ramadhan Abbas, ambapo walikagua maeneo mbalimbali ya uwanja huo na kujionea maandalizi yanayoendelea kuelekea hafla hiyo muhimu ya kidini.
Maulid ya Kitaifa yanatarajiwa kufanyika katika Uwanja wa Mnazi Mmoja usiku wa kesho Jumatatu, tarehe 24 Agosti 2026, huku waumini wa dini ya Kiislamu na wananchi kutoka maeneo mbalimbali wakitarajiwa kushiriki katika tukio hilo la kumuenzi na kumkumbuka Mtume Muhammad (saww).
Kwa mujibu wa ratiba ya maadhimisho hayo, siku inayofuata, Jumanne tarehe 25 Agosti 2026, kutakuwa na Baraza la Maulid litakalofanyika katika Ukumbi wa Mwalimu Nyerere, Posta jijini Dar es Salaam. Tukio hilo linatarajiwa kuwakutanisha viongozi wa dini, waumini na wageni mbalimbali katika kuendeleza ujumbe wa upendo, umoja, amani na mshikamano wa jamii.
Ziara ya Mufti Mkuu na viongozi wa BAKWATA imeelezwa kuwa ni sehemu ya maandalizi ya kuhakikisha hafla hiyo ya kitaifa inafanyika kwa utaratibu mzuri na inakuwa na mafanikio makubwa. Maulid ya Kitaifa ya mwaka huu yanatarajiwa kuwa fursa muhimu kwa Waislamu kukutana, kushirikiana na kuendeleza mafundisho mema ya Mtume Muhammad (saww) katika kuijenga jamii yenye amani, maadili na mshikamano.


Maoni yako