Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, matembezi hayo makubwa yalihudhuriwa na waumini kutoka maeneo mbalimbali ya Kenya, huku yakibeba ujumbe mzito wa kupinga dhulma na kuhuisha maadili na misingi aliyoisimamia Imam Hussein (as). Waumini walionekana wakipeperusha bendera za Imam Hussein (as) na mabango mbalimbali yaliyoakisi huzuni yao kutokana na madhila na dhulma zilizowakumba Ahlul-Bayt (as) mikononi mwa Yazid bin Muawiya.
Miongoni mwa mabango yaliyovutia zaidi katika maandamano hayo ni yale yaliyobeba maneno maarufu ya Imam Hussein (as): "Lengo langu ni kuamrisha mema na kukataza maovu." Ujumbe huo ulionekana kugusa hisia za washiriki wengi huku ukisisitiza umuhimu wa kusimama upande wa haki na kupambana na uovu katika jamii.
Aidha, hafla hiyo ilipambwa na hotuba na nasaha kutoka kwa Masheikh mbalimbali waliowakumbusha waumini nafasi na hadhi ya Imam Hussein (as) katika Uislamu, pamoja na kueleza kwa kina tukio la Karbala na namna mjukuu huyo wa Mtume (saww) alivyouawa kikatili akiwa katika harakati za kutetea dini, haki na utu wa mwanadamu.
Matembezi hayo pia yaliambatana na maonesho maalumu yaliyowasilisha baadhi ya matukio muhimu yaliyotokea katika ardhi ya Karbala, jambo lililowapa washiriki fursa ya kutafakari zaidi juu ya ukubwa wa msiba huo ulioitikisa historia ya Uislamu.
Katika kilele cha hafla hiyo, waumini walikusanyika kwa pamoja katika mazingira yaliyojaa hisia za maombolezo, ambapo waliimba tenzi na nyimbo za huzuni za kumbukumbu ya Imam Hussein (as), huku wakipiga vifua kuonesha mshikamano wao na ujumbe wa milele wa Karbala ambao unaendelea kuhamasisha vizazi kusimama dhidi ya dhulma na kutetea haki.
Matembezi hayo yameonesha kwa mara nyingine kuwa ujumbe wa Imam Hussein (as) bado unaishi katika nyoyo za mamilioni ya waumini duniani, na kwamba tukio la Karbala linaendelea kuwa chanzo cha mwamko, uadilifu na mapambano dhidi ya dhulma katika zama zote.







Maoni yako