Jumatano 22 Aprili 2026 - 00:15
Ayatollah Aṙāki amshukuru Papa Leo XIV kwa misimamo ya kishujaa/ Kufuata Injili maana yake ni kusimama dhidi ya dhana ya uongo ya nguvu za kibabe

Ayatullah Aṙāki katika barua aliyomwandikia Papa Leon XIV, kiongozi mkuu wa Kanisa Katoliki, ameandika: Wakati ulipotaja vitisho vya “kuangamizwa kwa ustaarabu mzima” na “uvamizi wa nchi nyingine” kuwa “visivyokubalika kabisa,” haukuwa ukitoa tu maoni ya kisiasa, bali ulitoa mwito wa dhamiri ya kimaadili ya wanadamu.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, maandishi ya barua ya shukrani ya Ayatollah Muhsin Aṙāki, mjumbe wa Baraza Kuu la Hawza na pia mjumbe wa uongozi wa Baraza la Wataalamu wa Uongozi, kwa misimamo ya kishujaa ya Papa Leon XIV, kiongozi mkuu wa Kanisa Katoliki, ni kama ifuatavyo:

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mtukufu

Mheshimiwa Papa Leon XIV
Kiongozi mkuu wa Kanisa Katoliki

Kwa heshima kubwa, ninakuandikia barua hii katika hali ambayo sauti yako yenye nguvu katika kutetea amani na uadilifu inang’aa kama taa katika giza la wachochezi wa vita na watawala wenye nguvu.

Katika dunia ambayo mantiki ya nguvu imechukua nafasi ya mazungumzo, na ambapo vitisho vya kuangamiza ustaarabu vimekuwa sera ya kawaida ya rais wa Marekani mwenye kiburi na dhalimu, wewe umeinuka kuwasaidia mamilioni ya watu wasio na ulinzi—wahanga wa vita, wakimbizi, na wamama waliopoteza watoto wao katika moto wa mabomu—na unasema kwa ajili ya kuwasaidia.

Wakati ulipotaja vitisho vya “kuangamizwa kwa ustaarabu mzima” na “uvamizi wa nchi nyingine” kuwa “visivyokubalika kabisa,” haukuwa ukitoa tu maoni ya kisiasa, bali ulitoa mwito wa dhamiri ya kimaadili ya wanadamu. Umeonesha kuwa kufuata Injili maana yake ni kusimama dhidi ya dhana ya uongo ya nguvu za kibabe, ambayo ndiyo chanzo cha vita na ukosefu wa usalama.

Kuchapishwa kwa picha bandia ya Donald Trump katika sura ya Masih (as), ni kitendo cha ukafiri na matusi kwa vitakatifu vya dini zote za mbinguni, na ni shambulio dhidi ya imani za mabilioni ya Wakristo na Waislamu duniani. Ulihimiza kwa usahihi kuwa “ujumbe wa Injili haupaswi kutumiwa vibaya.” Hatua hii inaonesha jinsi baadhi ya watawala wanavyoweza kufika mbali katika kupotosha ukweli na kuvunja heshima ya vitakatifu kwa ajili ya kujionesha na kupotosha fikra za umma. Lakini ukweli hauwezi kamwe kufichwa kwa uongo na matusi.

Mheshimiwa; umethibitisha kwamba uongozi wa Kanisa hauinamii mbele ya madhalimu wala haukai kimya kwa ajili ya kulinda maslahi ya kisiasa. Matusi na vitisho vya Trump havitikisi hadhi yako, bali vinaongeza juu ya hadhi na heshima ya misimamo yako. Historia itawakumbuka watu wa amani, si wale ambao kwa kutukana vitakatifu na kutishia ustaarabu hawajaacha isipokuwa aibu na fedheha.

Matusi ya Trump kwa kiongozi mheshimiwa wa Wakatoliki duniani kwa hakika ni matusi kwa mamilioni ya watu wanaotamani maisha ya kuishi kwa amani. Anafikiri kwamba kwa maneno makali anaweza kuzima sauti ya dhamiri; bila kutambua kwamba matusi hayo ni ushahidi wa ufisadi, uozo na udhalili wa anayetoa matusi, pamoja na uduni na maradhi ya nafsi yake.

Mwisho, kwa mara nyingine tena tunathamini na kushukuru msimamo wako huu wenye thamani, na tunamuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu alete uadilifu na amani katika dunia nzima.

Muhsin Aṙāki

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha