Jumamosi 5 Septemba 2026 - 07:24
Hoja 9 za Udhaifu na Kukosa Ustahimilivu kwa Marekani na Ubeberu Dhidi ya Mapinduzi ya Kiislamu / Kusimama Imara Taifa la Iran Kumeushangaza Ulimwengu Mzima

Hawza/ Khatibu wa Swala ya Ijumaa ya Qom amesema: Uwezo na nguvu ya taifa la Iran pamoja na uongozi wake katika kusimama imara dhidi ya ubeberu umeushangaza ulimwengu mzima. Wao hawakudhani kwamba taifa linaweza kusimama dhidi ya dola yenye nguvu kubwa zaidi duniani katika nyanja za kielimu, kiteknolojia, kiuchumi, kisiasa na kijeshi.

Kwa mujibu wa mwandishi wa habari wa Shirika la Habari la Hawza, Ayatullah Alireza Araafi katika hotuba za Swala ya Ijumaa ya tarehe 13 Shahrivar mjini Qom, iliyoswaliwa katika Muswalla ya Quds, alisisitiza umuhimu na ulazima wa kufanya uchambuzi kuhusu vita vya hivi karibuni vya kulazimishwa, akisema: Taifa lililoteuliwa kuwa mstari wa mbele ni taifa tangulizi, lakini kuendelea kufafanua masuala haya kwa kizazi cha leo na vizazi vijavyo kunaweza kuwa mwongozo. Kwa sababu mapambano ambayo tupo katikati yake ni mapambano yasiyo na mfano katika karne ya hivi karibuni kati ya Uislamu na kambi ya ubeberu.

Imam wa Swala ya Ijumaa ya Qom alisisitiza: Uwezo na nguvu ya taifa la Iran pamoja na uongozi wake katika kusimama dhidi ya ubeberu umeushangaza ulimwengu mzima. Hawakudhani kwamba taifa lingeweza kusimama dhidi ya dola yenye nguvu kubwa zaidi duniani katika nyanja za kielimu, kiteknolojia, kiuchumi, kisiasa na kijeshi.

Ayatullah Araafi alisema: Nguvu hii imetokana na Ijumaa, itikadi ya kusubiri na Mahdawiyya, umati mkubwa wa mashahidi na fikra za Imam Marehemu. Na hakuna sehemu yoyote duniani yenye jambo hili isipokuwa mahali palipojifunza kutoka kwenu. Hazina hii adhimu na safi inapaswa kulindwa.

Mkuu wa Hawza za Kiislamu nchini humo aliendelea kufafanua kuhusu maeneo ya udhaifu na kukosa ustahimilivu kwa Marekani na ubeberu mbele ya Mapinduzi ya Kiislamu.

Kwanza: Ustaarabu Uliojengwa Juu ya Dhuluma

Katika msingi wa ustaarabu wa Magharibi kuna dhuluma na ukandamizaji wa kihistoria. Mafanikio mengi ya Magharibi yamejengwa juu ya ukoloni wa Asia, Afrika na Mashariki. Historia inaonesha kwamba mizizi ya dhuluma na ukandamizaji imepenya katika misingi ya maendeleo ya kielimu na kiteknolojia.

Walipora madini ya Afrika na kuwafanya watu wake kuwa watumwa ili kuendeleza viwanda vya Uingereza, Ureno na nchi za Magharibi. Kasri lililojengwa juu ya msingi wa dhuluma huwa halina uimara.

Pili: Chuki ya Ulimwengu Dhidi Yao

Chuki ya dunia na kuchoshwa kwa ulimwengu na Magharibi yenye kuendekeza ubeberu ni kubwa kupita kiasi. Lakini watu pamoja na viongozi wakubwa hawana ujasiri wa kusema “Mauti kwa ubeberu” na “Mauti kwa Marekani”; kwa sababu hiyo walinyamaza.

Tatu: Uchumi Ulioendelea Lakini Wenye Utata

Uchumi wao na mifumo yao ya kiuchumi imepiga hatua kubwa, lakini maendeleo hayo yamezalisha mambo mengi magumu na yenye utata ambayo yamesababisha kuwa katika hali ya kukosa ustahimilivu.

Nne: Uchumi Uliojengwa Juu ya Ufisadi

Hata leo uchumi wao umejengwa juu ya ufisadi, ubaguzi na uporaji wa mali duniani. Kwa jeuri kubwa walimteka kiongozi wa Venezuela huku wakisema kwamba fedha za mafuta yao zinaingia katika akaunti zetu, wala hawaoni haya. Ufisadi huu umewafanya wawe dhaifu na wasiostahimili.

Aliendelea kusema: Hadi sasa hakuna aliyekuwa na uwezo wa kusimama mbele yenu, lakini leo taifa la Iran, Mapinduzi ya Kiislamu, mhimili wa Muqawama na Umma wa Kiislamu, kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, wamesimama mbele yenu.

Tano: Kuzama Katika Starehe na Kutokuwa na Uwezo wa Kuvumilia Mishtuko Mikubwa

Wao wamezama katika starehe. Ni starehe za uongo zenye misingi inayoyumba. Uwezo wao wa kustahimili na kuvumilia ni dhaifu sana, na jambo hili limewafanya wawe katika hali ya kukosa ustahimilivu.

Wamegongana na mwamba imara uitwao Muqawama na Mapinduzi ya Kiislamu. Trump mjinga leo amepoteza mwelekeo na hajui la kufanya.

Mkuu wa Hawza za Kiislamu nchini humo alisisitiza: Kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, tutawashangaza sana katika Mlango-Bahari wa Hormuz, Bab al-Mandab na maeneo mengine duniani.

Sita: Kutotufahamu

Kutokufahamu mbinu zetu mpya, mbinu za kivita ni udhaifu mwingine wenu, mmeona sehemu fulani, na sehemu nyingine pia mtaziona.

Saba: Kufungwa Mfumo wa Kisiasa wa Demokrasia ya Marekani

Marekani ina demokrasia ndani yake, lakini demokrasia yao imekwama kisiasa. Kuna sauti nyingi nchini Marekani ambazo hazina mahali pa kukimbilia, na jambo hili limewafanya wawe katika hali ya kukosa ustahimilivu.

Nane: Viwango Viwili

Saudi Arabia na Imarati, ambazo hazina uchaguzi wala demokrasia ya wananchi, ni vipenzi vya Marekani. Lakini nchi ambazo zina demokrasia ya wananchi zinachukiwa na Marekani. Viwango hivi viwili vimesababisha chuki ya ulimwengu mzima dhidi yao.

Tisa: Makosa ya Kimahesabu

Katika hotuba zilizotangulia tulitaja makosa 15 ya kimahesabu ambayo Marekani ilifanya katika vita vya hivi karibuni. Kosa la kwanza mlilolifanya ni kuhusiana na utawala wa Israel unaokalia nchi za watu kwa mabavu. Mioyo yetu inawaonea huruma wananchi wa Marekani kwa sababu baadhi ya watu wajinga na wenye mabavu wamewafanya kuwa mateka wa utawala huo mdogo unaokalia kwa mabavu wa Israel. Waliwadanganya ili muingie katika vita ambavyo mlijikuta mmekwama ndani yake.

Ayatullah Araafi aliendelea kusema: Maadui hawakuweza hata kuwatambua kwa usahihi wapinzani wa Mapinduzi ya Iran, wakadhani kwamba watu waoga wanaweza kuwa washirika wao. Hamkuutambua kwa usahihi ukubwa na utukufu wa Iran pamoja na vikosi vyake vya ulinzi na usalama.

Mkuu wa Hawza nchini Iran, aliwaambia maadui: Taifa la Iran na mantiki ya Iran yenye kujivunia heshima linawakamata. Aidha mrudi kwenye mantiki sahihi na ahadi sahihi, au jiandaeni kwa kuendelea mapambano ya Mwenyezi Mungu na msikie mwito wa: “Labbaika ya Rasulullah, Labbaika ya Hussein (as), Labbaika enyi Mashahidi na Labbaika ya Khamenei.”

Mjumbe wa Baraza la Walinzi la Jamhuri ya Kiislamu aliwakumbusha viongozi: Watambue thamani ya taifa, wajitahidi kutatua matatizo na wasonge mbele kwa ajili ya kulipiza kisasi cha damu hiyo takatifu na kufanya jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu. Viongozi na makundi yote wajifunze kutoka katika taifa hili na wasimame katika ahadi zao kwa taifa.

Alisema: Masuala ya kiutamaduni ni miongoni mwa misingi ya kuendeleza Mapinduzi ya Kiislamu. Usafi wa jamii, heshima na sitara, pamoja na kupunguza madhara ya kijamii, ni miongoni mwa mahitaji muhimu ya jamii. Sote tunapaswa kujitahidi kupunguza uchafu na maovu, na kulifanya jiji hili lenye nuru la Bibi Maasuma (as) kuwa safi zaidi.

Kanuni za Kushinda na Kuwa na Heshima Mbele ya Wageni

Ayatullah Araafi katika khutba ya kwanza, alipokuwa akifafanua kanuni za kuwa na heshima na kushinda mbele ya wageni, alisema: “Izzah” na “subira na Muqawama” ni miongoni mwa misingi ya msingi ya jamii ya Kiislamu katika kukabiliana na matatizo, matukio na hali ngumu.

Mkurugenzi wa Hawza nchini humo, huku akieleza kwamba heshima na subira ni siri ya kubaki imara na kumshinda adui, alisema: Subira na Muqawama vinapofikia kiwango kikubwa kijamii vinaweza kuleta miujiza kama vile siku 200 za ushujaa wa wananchi mitaani.

Mjumbe wa Baraza la Walinzi alitaja ufahamu na utambuzi wa kina kuwa sababu ya tatu, na kuongeza: Ufahamu na utambuzi wa kina vina nafasi muhimu katika uwezo wa kustahimili na kusimama imara mbele ya adui, kuvuka changamoto na vipindi vigumu katika njia ya taifa na Umma wa Kiislamu.

Imam wa Swala ya Ijumaa ya Qom aliendelea kusema: Mwenyezi Mungu katika Surat Yusuf anasema:

«قُلْ هَٰذِهِ سَبِیلِی أَدْعُو إِلَی اللَّهِ ۚ عَلَیٰ بَصِیرَةٍ أَنَا وَمَنِ اتَّبَعَنِی ۖ وَسُبْحَانَ اللَّهِ وَمَا أَنَا مِنَ الْمُشْرِکِینَ»

“Sema: Hii ndiyo njia yangu; ninamlingania Mwenyezi Mungu kwa uoni na utambuzi wa kina, mimi na anayenifuata. Na ametakasika Mwenyezi Mungu, wala mimi si miongoni mwa washirikina.”

Alisisitiza: Aya hii ina mihimili mitatu:

Mhimili wa Kwanza:

Wito wa Mtume wa Mwenyezi Mungu kuelekea kwenye malengo ya Mwenyezi Mungu, ikhlasi na tauhidi safi.

Ni wito wa kuelekea kwa Mwenyezi Mungu ambaye nguvu zote za ulimwengu ziko mikononi Mwake.

Mhimili wa Pili:

Wito wa Mtume (saww) si wito wa juu juu, wa kijinga au usio na utambuzi wa kina; bali ni wito unaojengwa juu ya akili, hekima, ufahamu na utambuzi wa kina.

Mhimili wa Tatu:

Wito huu hauishii na hauhusiani na kipindi fulani cha wakati; bali ni njia ya milele ambayo Mtume wa Mwenyezi Mungu (saww) ameifungua mbele ya mwanadamu, na baada yake wafuasi wake wanaendeleza njia hiyo.

Katika riwaya imekuja kwamba kauli «وَمَنِ اتَّبَعَنِی» inawahusu Imam Ali (as) na Maimamu (as). Lakini ni wazi kwamba wao ni viongozi wa harakati hii kuelekea kwa Mwenyezi Mungu na waanzilishi wa kuwaongoza viumbe kuelekea kwa Mwenyezi Mungu; hata hivyo, uongofu wa jamii haujaishia kwao pekee.

Akieleza kwamba njia hii imeendelea na leo imefikia kwenye Mapinduzi ya Kiislamu, aliongeza: Taifa lililoteuliwa kuwa mstari wa mbele na Umma wa Kiislamu wamekubali wito huu na wanaendelea kusonga mbele katika njia hii.

Imam wa Swala ya Ijumaa ya Qom alisema: Mwishoni mwa aya hii inasisitizwa:

«وَسُبْحَانَ اللَّهِ وَمَا أَنَا مِنَ الْمُشْرِکِینَ»

Yaani, katika njia ambayo Mtume wa Mwenyezi Mungu (saww) anaongoza kuelekea kwenye saada ya milele, Mwenyezi Mungu pekee ndiye kitovu chake. Lazima tuziunganishe nyoyo zetu na Mwenyezi Mungu pekee.

Akirejea aya isemayo:

«وَمَا یُؤْمِنُ أَکْثَرُهُمْ بِاللَّهِ إِلَّا وَهُمْ مُشْرِکُونَ»

“Na wengi wao hawamuamini Mwenyezi Mungu isipokuwa huku wakimshirikisha.”

Alisema: Miongoni mwa waumini, si wote wamefikia tauhidi safi na ikhlasi iliyo kamili. Wengi wanamuamini Mwenyezi Mungu, lakini kwa sababu imani yao si safi, imechafuliwa na aina za shirki zilizofichika; sambamba na kumwamini Mwenyezi Mungu, wanaamini pia vitu vyengine na nguvu nyingine.

Mkurugenzi wa Hawza za Kiislamu nchini humo alisema: Katika riwaya imekuja kwamba shirki zilizofichika ni za siri zaidi kuliko sisimizi mweusi anayekwenda juu ya mwamba mweusi katika usiku wenye giza. Yaani, kama ilivyo vigumu kumtambua sisimizi huyo, vivyo hivyo ni vigumu kutambua aina hii ya shirki.

Akirejea aya isemayo «أَدْعُو إِلَی اللَّهِ ۚ عَلَیٰ بَصِیرَةٍ», ambayo inasisitiza msingi wa utambuzi wa kina katika wito wa kuelekea kwa Mwenyezi Mungu na jihadi katika njia ya Mwenyezi Mungu, aliendelea kusema: Basar na basira ni vitu viwili tofauti, basari inahusiana na jicho la kimwili na milango ya nje ya hisia, wakati basira inahusiana na utambuzi wa ndani, nuru ya ndani, utambuzi wa kiakili na kutambua ugumu na tabaka mbalimbali za njia.

Mkuu wa Hawza nchini Iran, aliongeza: Katika lugha, imeelezwa kwamba basira maana yake ni akili au werevu. Fatanah na werevu vinatofautiana na utambuzi wa kawaida, fatanah maana yake ni utambuzi wa kina, kutambua mambo katika vipindi vigumu, kufahamu matabaka ya misiba na kutambua ukweli katika mazingira ya fitina.

Akieleza kwamba si watu wote wanaoweza kufahamu mambo kwa undani, alisema: Basira maana yake ni kuijua njia, kuitambua hoja, kutopoteza mwelekeo, na kutoruhusu vumbi na fitina kumfanya mtu ashindwe kuelewa hali halisi.

Khatibu wa Swala ya Ijumaa ya Qom aliongeza: Basira katika nyanja ya kiitikadi maana yake ni kumtambua Mwenyezi Mungu, kuitambua Akhera na Siku ya Kiyama, na kutoruhusu ulimwengu wa kimaada kumzuia mtu kuutambua ukweli wa uwepo. Hata hivyo, basira hii haitoshi kwa ajili ya kuifuata njia ya Mwenyezi Mungu katika nyanja za kijamii; bali lazima pia kuwe na basira ya kiutamaduni, kijamii na kisiasa.

Kutambua njia ya haki katika wito wa kuelekea kwa Mwenyezi Mungu, kutopotea katika sauti za kishetani na za kiibilisi, kutogharikishwa na vumbi na fitina zinazopigwa dhidi ya njia ya haki, ni msingi wa pili wa ukweli huu.

Alisema kwamba aya hii inaashiria basira ya kiitikadi pamoja na basira ya kijamii, na akaongeza: Imam Hussein (as) aliisoma aya hii mara kadhaa katika njia yake kuelekea Ashura ili kuonesha kwamba basira ina nyanja mbili:

Nyanja ya kwanza: Kumtambua Mwenyezi Mungu, kuifahamu Akhera na kuimarisha misingi ya itikadi;

Nyanja ya pili: Kutambua hoja na njia, kuifuata njia hiyo na kufahamu hila, njama na fitina.

Mkurugenzi wa Hawza nchini Iran, alikumbusha mwishoni: Basira katika uwanja wa mapambano, basira mbele ya adui, basira mbele ya hila za wenye kuhadaa, na kutomezwa na mikondo iliyoundwa na maadui ni miongoni mwa aina za basira.

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha