Kwa mujibu wa kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, licha ya hali ya hewa ya baridi, watu waliitikia wito wa mashirika kadhaa ya kiraia na kukusanyika katika Uwanja wa Odenplan katikati mwa Stockholm, kisha wakaandamana kupinga mipango ya Israel ya kuambatanisha sehemu za Ukingo wa Magharibi kwenye ardhi zinazokaliwa kwa mabavu.
Waandamanaji walitangaza rasmi upinzani wao dhidi ya mpango huo wa kuambatanisha, na wakataka kuchukuliwa hatua za haraka na za dhati kuhusu hali ya kibinadamu na mgogoro uliopo katika Ukanda wa Ghaza.
Jumapili iliyopita, utawala wa Israeli uliidhinisha mkataba wa kusajili ardhi za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi kama “umiliki wa Israel” kwa mara ya kwanza tangu kuikalia kwa mabavu ardhi hiyo mwaka 1967. Kwa mujibu wa Channel 7 Israel, hatua hiyo inajumuisha kufunguliwa kwa taratibu za kusajili ardhi zilizokuwa zimehifadhiwa hapo awali, kufutwa kwa sheria za zamani za Jordan kuhusu namna ya umiliki wa ardhi, pamoja na kufichuliwa kwa kumbukumbu za ardhi ambazo zimebaki siri katika miongo kadhaa.
Baadhi ya waandamanaji walibeba mabango yenye kaulimbiu kama vile “Simamisheni mauaji” na “Watoto wanauawa Ghaza.”
Segin Mader, mwanaharakati wa kisiasa wa Kiswiden aliyeshiriki katika maandamano hayo, alisema kuwa; wanaharakati wamekuwa wakiandaa maandamano ya kila wiki kwa zaidi ya miaka miwili.
Aliielezea hali ya Ghaza kuwa ni “janga la kibinadamu” na akaitaka serikali ya Sweden na jumuiya ya kimataifa kupitisha mpango mahsusi wa hatua.
Waandaaji wa tukio hilo walitangaza kuanzishwa kwa mpango mpya wenye anwani ya “Boykoti dhidi ya Israel,” unaowahimiza wafuasi kuishinikiza wabunge kuchukua msimamo mkali zaidi.
Chanzo: Anadolu Agency
Maoni yako