Jumatano 17 Septemba 2025 - 00:16
Uhalifu wa kikatili unaofanywa na utawala wa Kizayuni ni kofi la fedheha zaidi kwa nyuso za wale wanaodai kuheshimu Siku ya Kimataifa ya Demokrasia

Hawza/ Hujjatul-Islam wal-Muslimin Sayyid Sajid Ali Naqvi, kutokana na mnasaba wa Siku ya Kimataifa ya Demokrasia, katika ujumbe wake amesisitiza: Wakati ambapo Ghaza inateketea chini ya moto wa dhulma na uvamizi, dunia inazungumza kuhusu demokrasia, lakini mbele ya ukiukaji wa haki za mataifa imechagua kimya.

Kwa mujibu wa ripoti ya kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, sambamba na kuwadia Siku ya Kimataifa ya Demokrasia, Hujjatul-Islam wal-Muslimin Sayyid Sajid Ali Naqvi, Mwenyekiti wa Baraza la Wanazuoni wa Kishia Pakistan, katika ujumbe wake amesisitiza: Uhalisia wa demokrasia unaweza kupatikana pale tu ambapo kura na matakwa ya wananchi yanaheshimiwa, na mchakato huu uende sambamba na mafundisho ya Kiislamu.

Katika ujumbe huu imesema: Leo dunia inasherehekea Siku ya Demokrasia, lakini mbele ya maafa ya kibinadamu imechagua kunyamaza; Mashariki ya Kati, Ghaza inateketezwa chini ya moto wa dhulma na uvamizi; Ukingo wa Magharibi, mchakato wa mauaji na dhulma haujasimama; na Asia ya Kusini, mwenendo wa India dhidi ya mataifa na ukandamizaji wa haki za msingi za binadamu unaendelea, pamoja na hayo, kwa masikitiko makubwa, jumuiya ya kimataifa na hata Umoja wa Mataifa wamepuuzia ukweli huu.

Mwanachuoni huyu mashuhuri wa Kipa­kistani, akielekea kwenye muundo wa mifumo ya kisiasa iliyopo, ameongeza: Demokrasia iliyoenea duniani, kwa kiasi kikubwa imejengeka juu ya mfumo wa kibepari. Ingawa ndani ya mfumo huu vipo baadhi ya vipengele ambavyo kwa marekebisho na mapitio vinaweza kuwa na manufaa, lakini kwa masikitiko, katika nchi nyingi demokrasia imebaki kuwa kauli mbiu tu au neno lililoandikwa katika vitabu na nyaraka rasmi.

Akaendelea kubainisha: Kanuni ya msingi ya demokrasia ni utawala wa wananchi, kwa mkono wa wananchi na kwa ajili ya wananchi. Hata hivyo, katika nchi nyingi, kanuni hii imebaki katika maneno tu, uchaguzi hadi leo umekuwa daima ukiambatana na hofu na utata, na badala ya kutekeleza haki za msingi na uhuru wa kujieleza, zaidi umekuwa chombo cha kutumikia maslahi ya makundi binafsi.

Akaendelea kwa kunukuu falsafa ya kupewa jina la Siku ya Kimataifa ya Demokrasia: Siku hii kwa mara ya kwanza ilibainishwa mwaka 2008 kwa lengo la kuunga mkono demokrasia duniani kote na kuieneza katika nchi mbalimbali. Lakini swali la msingi ni hili: Je, hadi leo hatua yoyote madhubuti na ya kivitendo imechukuliwa katika njia hii? Tajiriba ya kihistoria inaonesha kwamba badala ya kuunga mkono demokrasia, mara nyingi madikteta ndiyo waliopata kuungwa mkono, na hilo lilitokana na maslahi ya kisiasa na kiuchumi ya nguvu kubwa.

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha