Kwa mujibu wa kitengo cha tarjuma cha Shirika la Habari la Hawza, katika kesi hiyo imeelezwa kuwa gereza la Oregon limekiuka waziwazi haki za wafungwa hao watatu wenye majina: Amirwadi Hassan, Niyaz Khushna na Hamza Jama.
Wafungwa hawa wamezuiliwa kupata chakula halali, na hata hawaruhusiwi kuswali sala za jamaa wakati wa sikukuu za Kiislamu wala kukutana na familia zao wakati wa sikukuu hizo.
Kinyume chake, wafungwa wa Kiyahudi, wenye asili ya Marekani (Native Americans), na Wakristo wanapewa chakula kinacholingana na dini zao na wanaruhusiwa kufanya ibada zao maalumu katika nyakati za sikukuu zao na hukutana na familia zao pia.
Waislamu hao wanadai haki ya kupewa heshima kwa sikukuu mbili kuu za Uislamu, yaani Idi al-Fitr na Idi al-Adh-ha, na kwamba gereza liheshimu suala la halali katika chakula, kwa maana ya chakula kisicho na nyama ya nguruwe wala pombe.
Ghadir Abbas, Naibu wa Baraza la Mahusiano ya Kiislamu na Marekani (CAIR), alisema: "Haya ni masharti ya msingi ya kuishi pamoja kwa watu wa dini mbalimbali ambayo ni lazima yaheshimiwe."
Hatimaye, mahakama ililitaka gereza hilo kuhakikisha linawapatia wafungwa Waislamu chakula halali cha kutosha, na kiwekwe kwa ajili ya wafungwa wote Waislamu wanaokiomba, na kuwapa ruhusa ya kutekeleza ibada za kidini za Kiislamu pamoja na kuwapatia vifaa vinavyohitajika kwa ajili ya ibada hizo. Aidha, wafungwa hao pia waliruhusiwa kukutana na familia zao.
Chanzo:KCBY
Maoni yako