Kwa mujibu wa ripoti ya kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, Bodi ya Usimamizi ya Sekretarieti ya Haram ya Imamu Husein (a.s), kwa kushirikiana na mshauri wa masuala ya kitamaduni wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iraq, walifanya ziara katika Ubalozi wa Vatikani mjini Baghdad.
Ujumbe huo ulikutana na Padre Charles Lwanga Suuna kwa ajili ya kufanya mazungumzo kuhusu kuimarisha ushirikiano wa kiutamaduni na kidini, pamoja na kueneza maadili ya pamoja.
Bwana al-Hasan Namah al-Khafi, Naibu Mkuu wa Idara ya Habari ya Haram, katika mazungumzo yake, alikumbusha ujumbe wa rambirambi wa kufariki kwa Papa Francis, na vilevile akataja mkutano wake wa kihistoria na kiongozi mkuu wa kidini wa Waislamu wa Kishia mjini Najaf kuwa ni hatua ya kihistoria katika zama hizi.
Ujumbe huo pia, kwa mnasaba huo, ulimpongeza Papa Leo wa 45 kwa kuteuliwa kwake kushika wadhifa mpya, na ukaeleza matumaini kwamba Papa atafanya ziara ya Karbala katika siku za usoni.
Pande zote mbili zilikazia umuhimu wa kuendeleza ushirikiano katika nyanja za kitamaduni na kibinadamu kwa ajili ya kuimarisha uelewano wa pande zote na maadili ya pamoja ya kibinadamu.
Maoni yako