Shirika la Habari la Hawza, – Ferentz Venturli, anayejulikana kwa jina la “Eterno” (“Milele”) katika mitandao ya kijamii, amechapisha video yake akionyesha akiirarua nakala ya Qur’ani Tukufu na kisha kuichoma moto. Alijihalalishia kitendo hicho cha kukufuru kwa kudai kuwa anapinga kile alichokiita “msimamo mkali wa Kiislamu.”
Venturli, ambaye hivi karibuni alijiunga na harakati ya kisiasa ya “Futuro Nazionale” (“Mustakabali wa Kitaifa”), inayoongozwa na Roberto Vannacci, mbunge wa Bunge la Ulaya, katika video yake ametoa wito wa “kuiokoa Italia kutokana na msimamo mkali wa Kiislamu.”
Roberto Vannacci, akijibu hatua hiyo, alisema kwamba; hamfahamu Venturli binafsi na kwamba yeye ni mmoja tu wa wanachama wa harakati hiyo. Alisisitiza kwamba harakati yake haitangazi wala kuhimiza kuwakejeli wafuasi wa dini na tamaduni nyingine, Marco Luzzi, ambaye ni afisa wa mkoa wa harakati hiyo ya kisiasa, pia alisema kuwa kitendo cha Venturli kilikuwa cha kibinafsi na kwamba kuna uwezekano wa kuchukuliwa hatua za kinidhamu dhidi yake.
Kulaaniwa na meya wa Reggio Emilia
Marco Massari, meya wa Reggio Emilia, alilaani kitendo hicho na kukielezea kuwa ni “cha kutukana na cha kibaguzi.” Aidha, alituma barua kwa jumuiya za Kiislamu za jiji hilo, akieleza mshikamano wake nao na kusisitiza umuhimu wa kuheshimu Qur’ani Tukufu kama rejea ya kiroho ya mamilioni ya Waislamu, pamoja na umuhimu wa kuheshimiana kwa ajili ya kuishi pamoja kwa amani katika jamii.
Suala hili pia limeibua radi amali nyingi katika mitandao ya kijamii, na kusababisha mijadala kuhusu Uislamu, Ukristo, uhamiaji na utambulisho wa kitaifa wa Italia.
Barua ya kulaani kudhalilishwa vitakatifu
Katika kuendelea kwa radi amali hizo, barua ya wazi kutoka kwa wanaharakati wa kiraia na wawakilishi wa jamii ya Kiislamu nchini Italia imechapishwa, ambapo kitendo dhidi ya Qur’ani Tukufu kimelaaniwa.
Waandishi wa barua hiyo wamesisitiza kwamba kulenga kudhalilisha vitakatifu vya kidini hakupaswi kuwa kisingizio cha kuchochea chuki na migawanyiko katika jamii. Aidha, wameeleza umuhimu wa kutenganisha kati ya “uhuru wa kujieleza” na “uchochezi wa chuki,” na kutoa wito kwa taasisi za kisiasa, kijamii na vyombo vya habari kushughulikia masuala ya kidini kwa uwajibikaji.
Barua hiyo pia imesisitiza umuhimu wa mazungumzo baina ya dini na tamaduni, kuheshimiana na kulinda amani ya kijamii. Aidha, imezitaka pande zote kujiepusha na miitikio inayoweza kuongeza mvutano au kupelekea vitendo vya vurugu, na kueleza malalamiko yao kwa mujibu wa sheria na kwa njia ya amani.
Maoni yako