Jumapili 6 Septemba 2026 - 11:05
Ayatullah A’rafi Abainisha Mambo 10 ya Kimkakati Kuelekea Mwaka Mpya wa Masomo ya Hawza/ Tuchukue Kiaga Cha Kulingania kwa Mwenyezi Mungu

Hawza/ Mkurugenzi wa Hawza nchini Iran, amesema kuwa Hawza zinapaswa kutekeleza ipasavyo jukumu lake la kihistoria kwa kutambua kwa usahihi mazingira ya zama, mahitaji ya jamii na mabadiliko yanayotokea duniani, na kuchukua hatua katika njia ya kufafanua mafundisho ya dini na kueneza ujumbe wa Uislamu.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Ayatullah Ali Reza A’rafi alitoa kauli hiyo kabla ya adhuhuri ya jana katika hafla ya ufunguzi wa mwaka mpya wa masomo ua Hawza, iliyofanyika katika Shule Tukufu ya Feiziyah mjini Qom Iran, akirejea aya tukufu isemayo:

«قُلْ هَٰذِهِ سَبِیلِی أَدْعُو إِلَی اللَّهِ ۚ عَلَیٰ بَصِیرَةٍ أَنَا وَمَنِ اتَّبَعَنِی وَسُبْحَانَ اللَّهِ وَمَا أَنَا مِنَ الْمُشْرِکِینَ»

alisema kuwa aya hii tukufu inaeleza mambo matatu muhimu ambayo kwa hakika ndiyo msingi ambao juu yake utambulisho wa Hawza na wanafunzi wa elimu za dini umejengwa.

Kuwalingania watu kwa Mwenyezi Mungu; nguzo kuu ya jukumu la Hawza

Alisema kuwa mhimili wa kwanza wa aya hii ni kuwaita watu kuelekea kwa Mwenyezi Mungu, akiongeza: Njia ya Mtume Mtukufu (saww) ilikuwa ni kuiita jamii na wanadamu kumuelekea Mwenyezi Mungu, na hii pia ni nguzo kuu ya jukumu na shughuli za Hawza.

Mkuu huyo wa Hawza aliendelea kusema: Mwanzoni mwa mwaka mpya wa masomo, sote tunapaswa kumuahidi Mwenyezi Mungu Mtukufu kwamba tutaendeleza njia hii; njia ambayo mwisho wake ni “kuelekea kwa Mwenyezi Mungu” na kuelekea kileleni na kwenye chanzo cha nguvu zisizo na kikomo za Mwenyezi Mungu.

Ayatullah A’rafi akisisitiza kwamba mamlaka kamili ya Mwenyezi Mungu juu ya mwanadamu na ulimwengu ndiyo msingi wa njia hii, alisema: Kuwalingania watu kuelekea kwa Mwenyezi Mungu maana yake ni kwamba harakati, shughuli na muelekeo wote wa mwanadamu upangwe kwa msingi wa Tauhidi na katika njia ya matakwa ya Mwenyezi Mungu.

Uelewa na utambuzi wa kidini; sharti la kutembea katika njia ya Mwenyezi Mungu

Mkurugenzi wa Hawza aliutaja “utambuzi” (basirah) kuwa mhimili wa pili wa aya hii tukufu, akasema: Mlingano huu unapaswa kuambatana na uelewa, utambuzi na basirah katika dini. Katika maneno ya wafasiri, neno “basirah” limefasiriwa kuwa ni ufahamu wa kina wa fiqhi, utambuzi wa kina na uelewa wa nyanja mbalimbali za dini; hivyo basi, Hawza inapaswa kuwa na basirah na uelewa wa kina kuhusu dini, njia yake na namna ya kuitekeleza na kuiweka katika vitendo ndani ya jamii.

Akirejea kwamba njia ya uongofu wa Mwenyezi Mungu haikomei kwa Mtume Mtukufu (saww), alisisitiza: Njia hii iliendelea kupitia uwepo wa Amirul-Muuminina (as) na Maimamu watoharifu (as), na baadaye wanazuoni wa dini, Marajii na Wilayat al-Faqih vimeendeleza njia hii ngumu.

Mkuu wa Hawza nchini Iran, alisisitiza kwamba; njia hii yenye nuru ni mfululizo wa kihistoria unaoendelea na ambao ulianza kwa Mtume Mtukufu (sawe), ukaendelea kupitia Uimamu wa Maimamu watoharifu (as), na katika historia yote ukaendelezwa na mafaqihi, wanazuoni na wakuu wa dini.

Ahadi ya wanafunzi wa Hawza kwa Mwenyezi Mungu ya kuendeleza njia ya Hawza ya miaka elfu moja

Ayatullah A’rafi akiwaelekea wanafunzi na vijana wa Hawza alisema: Utambulisho wetu na wenu, enyi wanafunzi wapendwa na vijana, unafafanuliwa ndani ya njia hii; ninyi wapendwa mlio hapa leo katika kituo hiki cha kielimu, jihadi na ushahidi wa kishahidi, yaani hawza ya Feiziyah, na vilevile marafiki na wanafunzi wote wapendwa wa Hawza wanaosikiliza maneno haya katika maeneo mbalimbali nchini, tunapaswa mwanzoni mwa mwaka mpya wa masomo kumuahidi Mwenyezi Mungu Mtukufu na Walii wa Asr (aj).

Aliendelea kusema: Tunapaswa kumuahidi kwamba, katika mwendelezo wa aya hii tukufu, ujumbe wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (sw) na Uimamu wa Maimamu watoharifu (as), tutaendeleza njia ya waliotangulia wema, mafaqihi na wakuu wa dini; watukufu ambao kwa zaidi ya miaka elfu moja wameubeba ujumbe huu wenye nuru na kuangaza jamii.

Mkuu wa Hawza, akirejea matatizo na mateso ambayo wanazuoni na mafaqihi waliotangulia walikumbana nayo katika njia hii, alisema: Wakubwa wa dini katika historia yote walivumilia matatizo na mashaka mengi kwa ajili ya kuhifadhi na kueneza maarifa ya Mwenyezi Mungu, na walijitoa mhanga katika njia hii. Leo urithi huu wenye thamani kubwa umekabidhiwa mikononi mwetu na mikononi mwenu.

Tuahidi kuwa miongoni mwa wanaotekeleza aya ya “أَدْعُو إِلَی اللَّهِ”

Ayatullah A’rafi alisisitiza: Tunapaswa kumuahidi Mwenyezi Mungu Mtukufu pamoja na wakubwa hawa wote kwamba tutakuwa miongoni mwa wanaotekeleza aya tukufu ya “أَدْعُو إِلَی اللَّهِ”; tuanze na “kuelekea kwa Mwenyezi Mungu”, tumuone Mwenyezi Mungu pekee, na tuelekeze mambo na masuala yote ya maisha yetu pamoja na shughuli zetu kuelekea Kwake. Njia hii inapaswa kuambatana na basirah na uelewa kuhusu dini; tunapaswa kujifunza Sheria kwa usahihi, kupata uelewa wa kina na sahihi wa mafundisho ya Kiislamu, na kuweza kueneza nuru ya Sharia duniani.

Mtazamo wa kimataifa wa jukumu la Hawza

Ayatullah A’rafi, akirejea jukumu la kihistoria la Hawza, alisema: Tunapaswa kuendeleza ahadi hii kwa ajili ya leo na kwa ajili ya mustakabali wa historia; kwa sababu leo macho ya watu wengi duniani yameelekezwa kwenye Hawza na uwezo wake.

Mjumbe wa Maimamu wa Baraza la Walinzi aliendelea kusema: Hawza zinapaswa kwa kutambua kwa usahihi mazingira ya zama, mahitaji ya jamii na mabadiliko ya dunia, kutekeleza ipasavyo jukumu lake la kihistoria na kuchukua hatua katika njia ya kufafanua mafundisho ya dini na kueneza ujumbe wa Uislamu.

Mambo 10 muhimu kwa mwaka mpya wa masomo wa Hawza

Jambo la Kwanza: Kuziba pengo la kielimu; kipaumbele cha kwanza cha Hawza

Mkurugenzi wa Hawza, akirejea baadhi ya matukio na misukosuko iliyotokea katika miaka na miezi iliyopita na kusababisha kuvurugika kwa mwenendo wa shughuli za kielimu na kisomi, alisema: Katika kipindi fulani tulikumbana na mambo kama vile Corona na vita vilivyolazimishwa, ambavyo kwa kiasi fulani vilisababisha usumbufu katika shughuli za kielimu, na huenda katika baadhi ya maeneo yakawa yamesababisha kuwepo kwa mapungufu ya kielimu. Mwaka huu ni muhimu kwa walimu, viongozi na wote wanaoshiriki katika shughuli za Hawza, kwa umakini, kuziba mapungufu hayo yanayoweza kuwa yamejitokeza. Ombi letu ni kwamba kuziba mapungufu ya kielimu kuwe miongoni mwa misingi mikuu ya mipango na shughuli za viongozi na walimu waheshimiwa wa Hawza.

Jambo la Pili: Hawza itakuwa pamoja na wananchi na Majeshi katika uwanja wa tukio

Aliendelea kusisitiza kuhusu msimamo wa Hawza kuhusiana na masuala ya Mapinduzi ya Kiislamu na kuilinda nchi, akasema: Wakati huo huo leo tunatangaza; kwa maadui wa Iran, Uislamu na Mapinduzi ya Kiislamu, na pia kwa marafiki zetu, kwamba Hawza bado inayapa kipaumbele Mapinduzi ya Kiislamu, kuwepo katika uwanja wa tukio na kusimama imara dhidi ya maadui wa Uislamu, Iran na Mapinduzi ya Kiislamu.

Mkuu wa Hawza alisisitiza: Ninawaomba viongozi na walimu waheshimiwa wa Hawza kwamba kila wanapohisi kuwepo katika uwanja wa tukio, mitaani na katika medani ni jambo la lazima kwa ajili ya kuyaunga mkono Majeshi na kuwaunga mkono wananchi, basi waweke uwepo huo kuwa kipaumbele.

Jambo la Tatu: Utayari wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kukabiliana na vitisho

Ayatullah A’rafi, akisisitiza kuhusu utayari wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kukabiliana na vitisho na mabadiliko mbalimbali, alisema: Ulimwengu mzima unapaswa kujua kwamba wananchi wa Iran, kwa kumfuata Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi ya Kiislamu, hawatapunguza juhudi hata kidogo katika njia ya kuendeleza Uislamu na Mapinduzi ya Kiislamu.

Mjumbe wa Baraza la Walinzi, akisisitiza juu ya kuambatana Hawza na wananchi wa Iran, na akirejea nafasi ya Mar'ajii Wakubwa wa Taqlidi katika kuiongoza Hawza, alisema: Kwa kuwafuata Mar'aji Wakuu wa Taqlidi, tupo pamoja na wananchi na tupo tayari kwa jambo lolote katika kukabiliana na adui.

Jambo la Nne: Kunufaika na mafunzo ya vita katika malezi ya kihawza na kijamii

Ayatullah A’rafi, alitaja kunufaika na mafanikio ya kiutamaduni, kimaadili na kimalezi ya vita vilivyolazimishwa kuwa miongoni mwa mihimili muhimu ya shughuli za Hawza, akasema: Tunapaswa kutumia mafanikio ya vita vilivyolazimishwa katika kuwaelimisha na kuwalea wanahawza, jamii, wanafunzi wa shule na wanafunzi wa vyuo vikuu.

Mjumbe wa Baraza Kuu la Hawza nchini Iran, aliongeza: Katika mkutano na Waziri wa Elimu nilisema kwamba, vita hivi vilikuwa kioo kamili cha imani ya taifa, na kwa hakika vilifungua mbele yetu kitabu na mkusanyiko wa mafunzo ya kimaadili na kimalezi. Walimu wetu ndani ya Hawza, Wizara ya Elimu na katika vyuo vikuu wanapaswa kuyafanya maonesho haya ya imani, kujitolea, kujitolea mhanga na kujitoa kwa wananchi na mashahidi kuwa msingi wa kitabu cha kutakasa nafsi na malezi.

Jambo la Tano: Kuimarisha nafasi ya Marjaiya na Wilayat al-Faqih

Mkurugenzi wa Hawza, akiendelea kueleza kuhusu nafasi ya Marjaiya na uongozi katika muundo wa Hawza, alisema: Marjaiya kama taasisi halisi ya Hawza inapaswa kupewa umuhimu na kuimarishwa, na hasa mwanzoni mwa uongozi wa Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi, mstari huu imara wa Hawza unapaswa kuendelezwa kwa nguvu. Sisi tuko pamoja na wakuu wa Hawza, na Wilayat al-Faqih ni mwanga unaotuongoza. Huu ndio mstari ulio wazi wa Hawza, na unapaswa kufuatwa kwa nguvu na uthabiti.

Jambo la Sita: Kufahamu fikra za Maimamu wawili wa Mapinduzi ya Kiislamu na wakuu wa dini

Ayatullah A’rafi alielezea kufahamu fikra za Imam Khomeini (ra), Kiongozi Shahidi wa Mapinduzi ya Kiislamu na wakuu wa Hawza kuwa miongoni mwa mihimili mingine ya msingi ya shughuli za Hawza, akasema: Kufahamu fikra za Imam alietangulia na wakuu wa Mapinduzi, hususan Maimamu wawili wa Mapinduzi, inapaswa kuwa miongoni mwa misingi mikuu ya shughuli za Hawza. Fikra za Imam alietangulia na Imam wetu Shahidi zinapaswa kupewa umuhimu mkubwa ndani ya Hawza, na kizazi kipya cha wanafunzi wa Hawza na wanazuoni wa dini kinapaswa kufahamishwa kwa kina na kwa kuendeleza misingi ya fikra, fikra za kisiasa, kijamii na kidini za Imam na viongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu.

Jambo la Saba: Jihadi ya kufafanua; jukumu la kudumu la Hawza

Mkuu wa Hawza za Elimu za Kidini aliitaja Jihadi ya kufafanua (Jihad al-Tabyin) na kutoa simulizi sahihi kuhusu Mapinduzi ya Kiislamu kuwa miongoni mwa majukumu muhimu ya Hawza, akasema: Jihadi ya kufafanua na kutoa simulizi sahihi kuhusu adhama ya Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran na duniani ni jukumu la muda wote kwetu sisi sote. Kila mmoja wetu anapaswa, kwa kiwango cha uwezo na nafasi yake, kuifahamisha jamii na dunia kuhusu ukubwa wa Mapinduzi ya Kiislamu, mafanikio yake na misingi ya fikra na thamani za harakati hii.

Ayatullah A’rafi alisisitiza: Hawza zinapaswa kuwa hai katika nyanja za kufafanua, kutoa mwangaza na kujibu shubha, na kwa kutumia uwezo wake wa kielimu, kifikra na tabligh, kutoa simulizi sahihi na zenye ushahidi kuhusu Mapinduzi ya Kiislamu na mabadiliko yanayotokea nchini.

Jambo la Nane: Nguvu ya kielimu na kifaqihi; mhimili mkuu wa Hawza

Mjumbe wa Baraza Kuu la Hawza nchini Iran, huku akisisitiza kwamba “kazi kuu ya Hawza ni nguvu yake ya kielimu, kifiqihi na kifikra,” alisema: Nguvu ya kielimu ya Hawza ni miongoni mwa misingi ya msingi ambayo haiwezi kupuuzwa.

Ayatullah A’rafi, akirejea historia ya kielimu ya Hawza, alisema: Katika historia yote tumekuwa na urithi mkubwa na wenye thamani katika nyanja za fikra, elimu ya Tawhidi na itikadi, Hadithi, tafsiri, fiqhi na elimu nyingine za Kiislamu, na msingi huu wa kina wa kielimu unapaswa kuhifadhiwa na kuimarishwa. Hawza inapaswa, sambamba na kuhifadhi urithi wake wenye thamani wa kielimu, kuweka mazingira ya ukuaji na maendeleo zaidi ya elimu za Kiislamu na isiruhusu msingi wa kielimu na kifkra wa Hawza kudhoofika au kuathirika.

Jambo la Tisa: Umuhimu wa mawasiliano endelevu kati ya Hawza na wananchi pamoja na kizazi cha vijana

Alitaja mawasiliano na wananchi na makundi mbalimbali ya jamii kuwa miongoni mwa vipaumbele vingine muhimu vya Hawza, akasema: Mawasiliano na wananchi, vijana, wanafunzi wa shule, wanafunzi wa vyuo vikuu, wasomi wa vyuo vikuu na matabaka yote ya jamii yanapaswa kuwa miongoni mwa mipango mikuu ya Hawza.

Ayatullah A’rafi, aliongeza: Hawza haiwezi kuwa isiyoijali jamii, masuala ya kizazi cha vijana na mabadiliko ya kifkra na kiutamaduni nchini. Wanazuoni na wanafunzi wa Hawza wanapaswa kuwepo miongoni mwa wananchi na kuimarisha mawasiliano yao na vizazi mbalimbali, hususan vijana, wanafunzi wa shule na wanafunzi wa vyuo vikuu.

Akirejea msisitizo wa Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi kuhusu Hawza inayoongoza na kuwa mfano wa ubora, alisema: Hawza inapaswa katika nyanja za kielimu, kiutamaduni, kijamii, kimahubiri na kimalezi kuwa Hawza inayoongoza, yenye ubora, yenye uhai na inayojibu mahitaji.

Jambo la Kumi: Kutumia teknolojia za kisasa huku ikihifadhi misingi ya Ijtihadi

Ayatullah A’rafi, katika sehemu nyingine ya hotuba yake, alisisitiza umuhimu wa Hawza kutumia mbinu na teknolojia za kisasa, akasema: Tunapaswa kutumia mbinu na teknolojia zote za kisasa kwa ajili ya kuendeleza Hawza na dini. Bila shaka, matumizi ya zana mpya yanapaswa kuambatana na kuhifadhi misingi sahihi ya Ijtihadi na mbinu za kina na zenye mizizi ya jadi ya Hawza.

Ayatullah A’rafi, alisisitiza: Hawza, sambamba na kushikamana na misingi yake halisi ya kielimu, kifaqihi na kiijtihadi, inapaswa kutumia uwezo wa teknolojia za kisasa kwa ajili ya kuendeleza elimu, utafiti, uenezaji wa dini, mawasiliano na jamii na kufikisha maarifa ya dini.

Mkurugenzi wa Hawza alihitimisha kwa kueleza matumaini yake akisema: Inshaallah, sisi sote tutakuwa askari wa Imam Jaafar Swa'diq (as) na Mtukufu Walii wa Zama (roho zetu ziwe fidia kwake), na tutaweza kuiendeleza njia ya Uislamu na Mapinduzi ya Kiislamu kwa usahihi, kwa basirah, elimu, maadili na roho ya kimapinduzi.

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha