Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Katika taarifa ya pamoja iliyotolewa Jumanne, wizara hiyo ilisisitiza kuwa waliotia saini wanakataa kwa uthabiti hatua za upande mmoja za Israel za kupanua uwepo wake katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu. Taarifa hiyo ilieleza kuwa, hatua hizo “zinakiuka wajibu wa Israel kwa mujibu wa sheria za kimataifa” na “zinapaswa kusitishwa mara moja.”
Nchi wanachama wa muungano huo pia zililaani mabadiliko yoyote katika “muundo wa idadi ya watu, asili na hadhi ya Ardhi ya Palestina inayokaliwa tangu 1967, ikiwemo East Jerusalem,” na kusisitiza upinzani wao mkali dhidi ya aina yoyote ya unyakuzi wa ardhi.
Taarifa hiyo ya pamoja ilithibitisha kujitolea kwao kwa “Azimio la New York” na kuchukua hatua mahsusi kwa kuzingatia sheria za kimataifa, maazimio ya Umoja wa Mataifa na maoni ya ushauri ya Mahakama ya kimataifa yaliyotolewa Julai 2024.
Muungano huo pia ulisisitiza “haki ya watu wa Palestina ya kujitawala,” na kutoa wito wa kupingwa sera za ujenzi wa makazi, vitisho vya kuwahamisha watu kwa nguvu na uporaji wa ardhi katika maeneo yanayokaliwa. Nchi hizo zilisisitiza tena kuwa; “amani ya haki na ya kudumu inaweza kupatikana tu kupitia utekelezaji wa suluhisho la mataifa mawili na kuundwa kwa Palestina huru na yenye mamlaka sambamba na Israel, ndani ya mipaka inayotambuliwa kimataifa kwa misingi ya mistari ya mwaka 1967.”
Hatua hii ya Brazil inaendeleza sera zake za hivi karibuni za kuunga mkono haki za Wapalestina. Hapo awali, serikali ya Brazil ililaani maamuzi ya baraza la usalama la Israel kuhusu kurahisisha “upatikanaji na uporaji wa mali katika Ukingo wa Magharibi,” ikiyataja kuwa yanakiuka sheria za kimataifa.
Aidha, mwezi Januari uliopita, Brazil ilieleza wasiwasi wake mkubwa kuhusu uharibifu wa makao makuu ya Wakala wa Misaada na Kazi wa Umoja wa Mataifa (UNRWA) huko Mashariki mwa Jerusalem, na kusisitiza uungaji mkono wake kwa kuendelea shughuli za shirika hilo kwa takriban wakimbizi wa Kipalestina milioni sita.
Msimamo wa serikali ya Luiz Inácio Lula da Silva, katika majukwaa ya kimataifa unaakisi kujitolea kwake kwa sheria za kimataifa, ulinzi wa raia na kuhakikisha taasisi za kibinadamu zinafanya kazi kikamilifu katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kimabavu.
Maoni yako