Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, hafla hiyo adhimu ya kisomo cha Qur’ani kwa mfumo wa Maqamat imeandaliwa na Hawza ya Imam Swadiq (as) iliyopo Kigogo Post, Dar es Salaam, ikiwa chini ya anuani isemayo: “Qur’ani Inatukusanya.” Kaulimbiu hiyo ilibeba ujumbe mzito wa mshikamano, umoja na kurejea kwa pamoja katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu kama dira ya maisha.
Lengo: Kuandaa Nyoyo kwa ajili ya mwezi wa Ramadhani
Mahafali hayo yalilenga kuandaa nyoyo za Waumini, kuupokea Mwezi mtukufu wa Ramadhani kwa ari mpya ya ibada, toba na kujikurubisha zaidi kwa Mwenyezi Mungu. Kupitia sauti tamu na zenye kugusa nyoyo za wasomaji mahiri wa Qur’ani, washiriki walipata fursa ya kutafakari aya za Mwenyezi Mungu katika mazingira ya kiroho yaliyojaa utulivu na taadhima.
Viongozi wa Kidini Wahudhuria
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kidini na kijamii. Miongoni mwao alikuwepo Sheikh Mkuu wa Jumuiya ya Shia Tanzania (TIC), Maulana Sheikh Hemedi Jalala, ambaye alikuwa mwenyeji wa hafla hiyo, huku akisisitiza umuhimu wa Qur’ani katika kujenga maadili na kuimarisha mshikamano wa jamii.
Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa ni Sheikh Ali Ngeruko, Naibu Qadhi Mkuu wa Tanzania Bara na mjumbe wa Baraza la Ulamaa la BAKWATA, ambaye alitoa nasaha zenye kugusa nyoyo kuhusu nafasi ya Qur’ani katika maisha ya Muislamu, hususan katika mwezi wa Ramadhani.
Qur’ani – Chemchemi ya Umoja na Mwanga
Mahafali hayo yameacha athari chanya kwa washiriki, yakionesha wazi kuwa Qur’ani Tukufu si tu Kitabu cha kusomwa, bali ni mwongozo kamili wa maisha unaowaunganisha Waumini chini ya mwamvuli wa imani, maadili na mshikamano.
Kwa hakika, tukio hili limekuwa mwanzo mzuri wa safari ya kiroho kuelekea Ramadhani, likiwahimiza Waumini kuingia katika mwezi huo mtukufu wakiwa na nyoyo safi, nia thabiti na mapenzi ya dhati kwa Qur’ani Tukufu.









Maoni yako