Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Ayatullah Mahdavi-Pour aliwasili akiwa ameambatana na Balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran nchini Tanzania pamoja na Mkurugenzi wa Utamaduni wa Iran. Ugeni huo uliifanya ziara hiyo ikiwa sehemu ya juhudi za kuimarisha mahusiano ya kirafiki na ushirikiano katika nyanja mbalimbali, hususan katika eneo la elimu na mahusiano mema ya kitaasisi.
Ziara hiyo pia imekuwa fursa muhimu ya kuimarisha udugu, maelewano na mahusiano mema kati ya taasisi za kidini na kielimu za Tanzania na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, sambamba na kuangalia namna ya kuendeleza juhudi za pamoja katika sekta ya elimu, malezi na huduma kwa jamii.
Akizungumza wakati wa kupokea ugeni huo, Maulana Sheikh Hemed Jalala Mwakindenge aliupongeza ugeni huo na kueleza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano kati ya taasisi hizo, huku akisisitiza kuwa elimu ni msingi muhimu wa maendeleo na ustawi wa jamii.
Sheikh Hemed Jalala amesema: Ushirikiano wa kielimu unapaswa kuendelea kupewa kipaumbele, kwa kuwa una nafasi kubwa katika kujenga kizazi chenye maarifa, maadili na uwezo wa kuchangia maendeleo ya jamii, Tanzania na ulimwengu wa Kiislamu kwa ujumla.
Ziara hiyo imehitimishwa kwa kusisitiza umuhimu wa kuendeleza mawasiliano, udugu na ushirikiano wa taasisi za kidini na kielimu, kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.



Maoni yako