Kwa mujibu wa Kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, kwa kunukuu kutoka katika tovuti ya RT ya Urusi kutoka gazeti la Zaman la Uturuki, Tommaso Bortolazzi, mwanaharakati wa Kiitaliano aliyekuwa ndani ya Flotilla ya Sumuud, baada ya kukamatwa na vikosi vya Israeli, alitangaza kwamba ameingia katika dini ya Uislamu.
Katika mahojiano yake na kituo cha televisheni cha TRT cha Uturuki kwenye Uwanja wa Ndege wa Istanbul, alisema:
“Safari hii ilianza kutokana na upendo wangu kwa watu wa Palestina, na ule ulikuwa wakati sahihi wa kufanya uamuzi.”
Bortolazzi alielezea hali ya kukamatwa kwake karibu na Ghaza, mahali ambapo mateso ya pamoja yalianza. Alisema kwamba katika siku tatu za kifungo, walikumbana na ukatili, kunyimwa maji, usingizi na mahitaji ya msingi.
Alitaja tukio maalum ambalo lilikuwa hatua ya mabadiliko kwake, alipokuwa katika jela ya pamoja na wanaharakati wanane Waislamu kutoka Uturuki na Malaysia, aliamua kusilimu. Bortolazzi alisema:
“Asubuhi moja walipokuwa wakiswali, polisi walivamia kizimba. Niliona tukio hili kuwa la kinyama na nikajaribu kulikemea. Hilo lilikuwa ni mshambulio dhidi ya imani yao. Baada ya hapo, nilizungumza na marafiki zangu, nao walipendekezea nitamke shahada. Nilihisi kuwa huo ndio mwelekeo sahihi, na kwa sababu ya upendo wangu kwa watu wa Palestina, nilisilimu.”
Alisisitiza kuwa hatua yake ya kwanza baada ya kurejea Rome itakuwa ni kwenda msikitini ili kuhalalisha rasmi imani yake.
Bortolazzi aliitaka serikali ya Italia ichukue msimamo mkali dhidi ya kuiunga mkono Israeli, na akaeleza kwamba kusitisha uuzaji wa silaha ni lazima iwe sehemu ya hatua za kivitendo.
Maoni yako