Kwa mujibu wa taarifa ya Idara ya Habari za Kimataifa ya Shirika la Habari la Hawza, katika kulaani jinai za hivi karibuni za utawala wa Kizayuni na kwa mshikamano na wananchi wanyonge wa Palestina na Ukanda wa Ghaza, hafla ya kumbukumbu ya mashahidi wa Quds na mapambano ilifanyika huku ikihudhuriwa na Sheikh Ibrahim Zakzaky, pamoja na umati mkubwa wa wanazuoni, waandishi wa habari na wananchi kutoka madhehebu na makabila mbalimbali mjini Abuja, mji mkuu wa Nigeria. Hafla hii iliandaliwa katika makazi ya Sheikh Ibrahim Zakzaky, kiongozi mashuhuri wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria.
Katika mkutano huo, Sheikh Zakzaky, kupitia hotuba yake, alionesha chuki kali dhidi ya vitendo vya kinyama vinavyofanywa na utawala ulio ikalia Quds na kulaani jinai za utawala huu dhidi ya watoto na raia wasio na hatia, na kusisitiza juu ya dhulma inayowakumba wananchi wa Ghaza na mapambano ya kishujaa ya wapiganaji wa Palestina. Akiashiria umuhimu wa hadhi ya Quds na watu wa Palestina, aliwatambulisha wao kuwa ni alama ya mapambano na imani kwa jamii yote ya Kiislamu.
Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria pia katika sehemu ya hotuba yake alikosoa ukimya wa baadhi ya viongozi wa Kiislamu kuhusu matukio yanayoendelea na akasema: "Bayt al-Maqdis ni ardhi takatifu inayounganisha mioyo ya Waislamu wote. Kila mtu anayeamini kwa Mwenyezi Mungu na Siku ya Kiyama, hana budi kuwa na wasiwasi juu ya hatima ya Quds."
Sheikh Zakzaky mwishoni mwa hotuba yake aliwataka Waislamu wawe macho na wastahimilivu katika kuutetea mji mtakatifu wa Quds na maeneo mengine matakatifu yaliyokaliwa kimabavu, na akasisitiza juu ya ulazima wa mshikamano katika sekta hii.
Maoni yako