Ijumaa 13 Februari 2026 - 23:00
Kongamano la Milenia ya Hawza ya Kielimu ya Najaf Ashraf Lafikia Tamati; Tafiti Mbili Zawasilishwa katika Kikao cha Mwisho

Hawza/ Siku ya mwisho ya kikao cha awali cha siku mbili cha kongamano la kwanza la kielimu la kuadhimisha milenia ya Hawza ya Kielimu ya Najaf Ashraf ilihitimishwa kwa kuwasilishwa tafiti mbili za kimataifa na kuwatunuku watafiti.

Kwa mujibu wa Kitengo cha Kimataifa cha Shirika la Habari la Hawza, tarehe 12 February kikao cha cha mwisho cha siku ya pili ya kikao cha awali cha kongamano hilo kilianza kwa kusomwa aya za Qur’ani Tukufu, na kumalizika kwa kuwasilishwa tafiti mbili za kimataifa, hotuba za ujumbe kutoka nje ya Iraq na kamati ya maandalizi, pamoja na hafla ya kuwapongeza watafiti.

Utafiti wa kwanza

“Karibu atawale”; mijadala ya Amirul-Muuminin Imam Ali (a.s) na wajumbe wa baraza la uteuzi wa ukhalifa katika turathi za Kisunni na Kishia

Utafiti huu uliandikwa na Nabil Husayn kutoka Marekani, ukichambua riwaya iliyopo katika kitabu Amaalī cha Shaykh al-Tusi. Riwaya hiyo inaeleza jinsi Imam Ali (a.s) alivyowalazimisha watu watano wa baraza lililoteuliwa na Umar ibn al-Khattab kukiri ubora wa daraja na fadhila zake juu ya wengine.

Mtafiti anaeleza kuwa baada ya kifo cha Umar ibn al-Khattab, baraza la watu sita kutoka miongoni mwa Masahaba liliundwa kwa ajili ya kumchagua khalifa wa tatu. Riwaya katika vyanzo vya Sunni na Shia zinaonesha kuwa kulikuwa na mazungumzo na hoja kati ya Imam Ali (a.s) na wajumbe wa baraza, ambapo alisisitiza kustahiki kwake zaidi ukhalifa.

Hoja hiyo ilitokea wakati Abd al-Rahman ibn Awf alipompendekezea Imam Ali (a.s) kuongoza Waislamu kwa sharti la kushikamana na Qur’ani Tukufu, Sunna ya Mtume na mwenendo wa masheikh wawili. Imam alikataa sharti hilo, lakini Uthman ibn Affan alilikubali.

Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti huu, baadhi ya wanazuoni wa Kisunni wamenukuu sehemu chache tu za riwaya ya Amr ibn Hammad Qannad (aliyefariki 222 H/837 M), ilhali Sheikh Tusi katika kitabu al-Amaalī ameileta riwaya hiyo kwa ukamilifu au karibu na ukamilifu.

Utafiti wa pili

Kitabu “Misbah al-Mutahajjid” cha Sheikh Tusi na athari yake katika turathi za kielimu za Shia

Fini Khitia, mtafiti kutoka Marekani, katika utafiti huu alichunguza vipengele viwili muhimu vinavyohusiana na kitabu Misbah al-Mutahajjid cha Sheikh Tusi:

Kipengele cha kwanza: namna maandishi hayo yalivyopokelewa na kusambazwa katika historia, ikiwemo riwaya zake, mzunguko wa nakala na maandishi ya mkono. Utafiti unaonesha kuwa turathi za msingi za kitabu hiki zinaonekana wazi katika sehemu nyingi za kielimu na maelezo ya pembeni ya mapema, tangu wakati wa uandishi wake hadi kipindi cha Safawi, jambo linaloashiria umuhimu wake mkubwa na uaminifu waliokuwa nao miongoni mwa wanazuoni wa Kishia katika karne mbalimbali.

Kipengele cha pili: kufafanua baadhi ya mada kuu zilizomo ndani ya kitabu hicho, hususan uwiano kati ya ibada kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu na kuonesha mapenzi na wilaya kwa Maimamu kumi na wanne (a.s). Kwa mujibu wa mtafiti, muunganiko sahihi wa mada na aina mbalimbali za ibada katika kitabu hiki unaonesha nafasi yake katika kuunda mtindo wa maisha ya kiibada ya Mashia katika kipindi cha miaka elfu moja baada ya kuandikwa kwake.

Mtafiti alisisitiza kuwa Misbah al-Mutahajjid imechangia wazi katika kuunda mtazamo maalumu wa uchamungu wa Kishia na kukuza mtindo wa maisha ya kidini kwa watu wa kawaida na wanazuoni wa Shia; mtindo uliopangwa kwa misingi ya saa, siku na miezi, ukitoa mfumo maalumu wa ibada.

Hotuba za ujumbe wa kimataifa na kamati ya maandalizi

Kongamano hili pia lilishuhudia hotuba za mwisho kutoka kwa ujumbe wa washiriki waliotoka nje ya Iraq. Walishukuru mapokezi mazuri na ukarimu walioupata, wakasifu juhudi za kielimu na za kiutawala zilizofanikisha tukio hilo, na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza mawasiliano ya kielimu kati ya taasisi na vituo vya utafiti.

Kamati ya maandalizi ya kongamano nayo katika hotuba yake ya mwisho ilieleza hatua muhimu za maandalizi, ikitaja ushirikiano wenye matokeo kati ya taasisi zilizosaidia na kamati mbalimbali zilizoshiriki. Kamati hiyo ilipongeza ushiriki wa watafiti na wageni, na kueleza matumaini kuwa matokeo ya kongamano yatatumika katika kuimarisha harakati za kielimu.

Kuwatambua watafiti walioshiriki

Katika mwendelezo wa kikao hicho, Ataba Tukufu ya Hadhrat Abbas (a.s) iliandaa hafla maalumu ya kuwapongeza watafiti walioshiriki katika vikao vya kielimu. Hatua hiyo ilifanyika kwa lengo la kuthamini juhudi zao katika kuandaa tafiti za kisayansi ambazo zimeongeza utajiri wa maudhui ya kongamano na kubainisha vipengele vya kifikra na maarifa vya mada yake.

Katika hafla hiyo, umuhimu wa nafasi ya watafiti katika kuimarisha harakati za kielimu na kufufua turathi za kifikra za Hawza ya Najaf Ashraf ulisisitizwa, na juhudi zao zikatajwa kuwa ni hazina ya kudumu kwa mustakabali wa tafiti za Kiislamu. Pia tukio hilo lilionekana kuwa ishara ya kuthamini hadhi ya kielimu na kiroho ya watafiti na kutambua mchango wao katika kuhudumia elimu na utamaduni wa Kiislamu.

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha