Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza kutoka Sa'ri Iran, hafla ya kuanza mwaka mpya wa masomo wa 1405–1406 wa Hawza za Mkoa wa Mazandaran ilifanyika tarehe 21 Shahrivar, huku Ayatullah Shabzandari akihutubia, hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Hujjatul-Islam wal-Muslimin Muhammadi La’ini, mwakilishi wa Waliyyul-Faqih katika Mkoa wa Mazandaran; Hujjatul-Islam wal-Muslimin Sadrullah Ismailzadeh, Mkuu wa Hawza za Mkoa wa Mazandaran; pamoja na viongozi mbalimbali wa Hawzah na mkoa, hafla hiyo ilifanyika katika Madrasa ya Imam Sadiq (as), Kotena Qa’imshahr.
Ayatullah Shabzandari katika hafla hiyo ya kuanza mwaka mpya wa masomo wa Hawza za Mkoa wa Mazandaran alisema: “Wanadamu ambao maumbile yao ya kibinadamu hayajazimwa na ambao hawajaathiriwa na mambo mbalimbali, hutafuta majibu ya swali hili: Tunawezaje kufikia lengo letu la mwisho? Na mafundisho haya ya kiroho ya uongo pia yamejitokeza kwa sababu ya watu hawa wapendwa wanaotafuta jibu la swali hilo.”
Aliendelea kusema: “Ili kufikia mafanikio ya milele, Mwenyezi Mungu ameweka mambo matatu kuwa muhimu, jambo la kwanza ni taqwa: ‘اتقوا الله’. Taqwa imeelezwa katika hadithi kwa namna hii:
یراک الله فیما یطلبه و لا یراک فیما ینهی عنک
yaani, Mwenyezi Mungu akuone ukiwa katika kila uwanja ambao amekutaka uwepo, na katika kila sehemu aliyokukataza, asikuone ukiwa humo. Mtu anayetekeleza jambo hili katika maisha yake huhesabiwa kuwa miongoni mwa wachamungu.”
Katibu wa Baraza Kuu la hawzah aliitaja taqwa kuwa sharti la msingi la kufikia daraja za juu, na kuongeza: “Jambo la pili ni kwamba, sambamba na taqwa, mtu anapaswa ‘kutafuta njia ya kumfikia Mwenyezi Mungu’ (ابتغاء وسیله). Yaani, pamoja na taqwa hii, mtu anapaswa kuomba msaada kupitia nuru tukufu za Maimamu Maasumina (as), ili kufikia malengo ya juu.”
Ayatullah Shabzandari alisema: “Sambamba na taqwa, kunapaswa kuwepo mapenzi ya kweli na ya kina kati yetu na Ahlul-Bayt (as), na katika kuwapenda tusiweke mipaka ya kujitolea. Njia hii inapowekwa pamoja na taqwa, huinua thamani ya kiroho ya mwanadamu.”
Mjumbe wa Jumuiya ya Walimu wa Hawza ya Qum, huku akizungumzia njama za maadui katika kipindi chote cha Mapinduzi ya Kiislamu, alisema: “Tumeona kwa macho yetu mambo mengi yakitokea katika nchi hii, lakini uhusiano na Ahlul-Bayt (as) uliyayeyusha yote hayo.”
Mwalimu wa Hawza ya Qum, akieleza kwamba mapenzi ya dhati kwa Ahlul-Bayt (as) yamewasukuma watu katika kuilinda serikali na Mapinduzi, aliwaambia wanafunzi wa Hawzah: “Ili kufikia kilele cha kujitakasa na kujijenga kiroho, msipuuze kutafuta msaada na kumtegemea Mwenyezi Mungu kupitia nuru hizi tukufu.”
Mjumbe wa wanazuoni wa Baraza la Walinzi alikumbushia baadhi ya mifano ya wanazuoni na watu wakubwa wa Hawzah waliokuwa wakitafuta msaada wa Ahlul-Bayt (as), na kuwaambia wanafunzi vijana: “Juweni kwa yakini kabisa kwamba ikiwa mtawaomba msaada kwa moyo wa dhati kabisa yeyote miongoni mwa nuru hizi tukufu, hasa Hadhrat Baqiyatullah al-A’dham (aj), mtapata jibu.”
Katika sehemu nyingine ya hutuba yake alisema: “Mwenyezi Mungu katika zama hizi, kwa baraka ya uelewa wa kina na mwanga wa fikra wa Imam Khomeini (q.s.) na juhudi za kiongozi shahidi wa Mapinduzi, na leo kupitia uongozi wa Ayatullah Sayyid Mujtaba Khamenei, ameipa nchi hii kile ambacho ni matarajio ya Mashia, yaani serikali ya Kiislamu; hivyo, jukumu la Hawza katika kulinda Mapinduzi haya ni kubwa na zito sana.”
Ayatullah Shabzandari alisema: “Hawzah inayotarajiwa na Imam Sadiq (as) na Imam Mahdi (aj) ni Hawzah yenye kukidhi mahitaji katika nyanja zote, hawzah ambayo ndani yake kuna elimu zote zinazohitajika na jamii—iwe ndani ya nchi au katika uwanja wa kimataifa. Hili linahitaji kusoma kwa usahihi, kujifunza mbele ya walimu wenye uwezo mkubwa na kushikamana na taratibu za Hawzah ambazo zimejaribiwa na kuthibitika.”
Mwalimu wa Hawza ya Qum, huku akizungumzia utamaduni wa kujadiliana masomo, maandalizi ya masomo kabla ya darasani na kurejea katika mijadala iliyopita, alisisitiza: “Msiruhusu uzoefu wa Hawza na mambo ambayo yamekuwa sababu ya maendeleo na malezi ya watafiti mashuhuri kutoweka.”
Aidha, alisema kuwa jamii inahitaji wanazuoni wenye taqwa na wanaojali watu, akisisitiza: “Watu wanapaswa kuelewa kwamba mwanazuoni huyu hajafungamana na dunia na kwamba anawajali watu. Mwanazuoni mwenye taqwa na anayewajali watu anaweza kuongoza mkoa mzima.”
Katibu wa Baraza Kuu la Hawza, huku akizungumzia kusitishwa masomo ya Hawza wakati wa vita vilivyolazimishwa mara ya tatu, alisema: “Iwapo kuanzishwa Mapinduzi ya Kiislamu kulifanywa na wanazuoni wa dini, basi kuendelea na kudumu kwake pia kunapaswa kuwa jukumu la wanazuoni hao. Hawzah wakati wa vita iliamua kwamba uwepo mitaani ulikuwa na kipaumbele kuliko kusoma; lakini Inshaallah, mipango iwekwe kwa namna ambayo ‘kulinda mfumo na Mapinduzi’ na ‘kusoma wanafunzi wa Hawzah’ vitakuwa vipaumbele viwili muhimu vya Hawzah.”
Hujjatul-Islam wal-Muslimin Muhammadi La’ini, mwakilishi wa Waliyyul-Faqih katika Mkoa wa Mazandaran, pia katika hafla hiyo, huku akirejelea aya za 144 na 145 za Surat Al-A’raf, alisema: “Hawzah ni mahali pa kuelewa na kufahamu ujumbe na maneno ya Mwenyezi Mungu, na kuwafikishia watu.”
Imam wa Swala ya Ijumaa wa Sari, akizungumzia umuhimu wa kujitakasa na kujipamba kwa maadili mema ndani ya Hawzah, aliongeza: “Tunapaswa kujivunia kwamba, miongoni mwa idadi hii kubwa ya watu, Mwenyezi Mungu ametuchagua sisi ili tuelewe maneno Yake na kuwafikishia watu.”
Akizungumzia wanafunzi wa Hawzah na wanazuoni waliouawa kishahidi, alisema: “Tunatumaini kwamba Mwenyezi Mungu atatuandikia hatima hiyo hiyo ya kufa kishahidi, au atujaalie tufuate njia ya malengo na matarajio yao.”
Maoni yako