Kwa mujibu wa kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, Hujjatul-Islam wal-Muslimin Sheikh Ali Al-Khatib, Naibu Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Kiislamu la Shia la Lebanon, alifanya ziara ndani ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Iraq iliyodumu kwa siku 11. Katika kipindi hicho, alishiriki katika Mkutano wa 40 wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu uliofanyika Tehran na Mashhad, na akafanya mfululizo wa mikutano katika nchi hizo mbili na viongozi mbalimbali rasmi wa kisiasa na wa kidini. Miongoni mwao walikuwa ni Waziri Wakuu wa Iraq Ali Al-Zeidi, na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araqchi. Sheikh Al-Khatib alihitimisha ziara yake kwa kukutana na Sheikh Hammam Baqir Hamoudi, Mwenyekiti wa kundi la wabunge la “Abshir Yā Iraq”, na kumjulisha kuhusu maendeleo ya hali nchini Lebanon, hususan kusini mwa Lebanon, katika kivuli cha mashambulizi yanayoendelea ya Israel.
Sheikh Al-Khatib alisema: “Nilifanya ziara yenye mafanikio ndani ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Jamhuri ya Iraq, ambapo tulishiriki katika Mkutano wa 40 wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu kwa mwaliko wa Baraza la Dunia la Kuleta Ukaribu baina ya Madhehebu ya Kiislamu. Tulipewa nafasi ya kutoa hotuba katika kikao cha ufunguzi, ambapo tulijadili fikra za Imam Shahidi Khamenei. Pia tulishiriki katika vikao vya mkutano, ambapo tuliheshimiwa kwa kuteuliwa kuwa miongoni mwa wajumbe wa Baraza Kuu na Kamati ya Kielimu ya mkutano huo.”
Aliongeza: “Pembeni mwa mkutano huo, tulifanya mfululizo wa mikutano na viongozi kadhaa wa kisiasa na kidini wa Iran kutoka Tehran, Qom na Mashhad. Vilevile, tulifanya mikutano kama hiyo nchini Iraq, katika miji ya Baghdad, Najaf na Karbala. Miongoni mwa mikutano muhimu zaidi ilikuwa ule na Waziri Mkuu wa Iraq, Ali Al-Zeidi. Tuliwaeleza viongozi hao kuhusu hali nchini Lebanon, hususan kusini mwa Lebanon ambako mashambulizi ya ‘Israel’ yanaendelea, pamoja na mateso ambayo watu wetu wanayapata. Tuliomba uingiliaji katika nyanja zote ili mashambulizi haya yakomeshwe, kuondoka kwa majeshi ya Israel kuwe na uhakika, na watu wetu waweze kurejea katika miji na vijiji vyao.”
Akaongeza: “Kwa viongozi hawa tuliona utayari kamili wa kutusaidia katika nyanja zote za kisiasa, kiuchumi na kijamii; kama vile tulivyoona juhudi zao za kuunga mkono umoja wa Lebanon pamoja na makundi yake yote. Katika hatua ijayo, tunatumaini kwamba utayari huu utatafsiriwa kuwa vitendo halisi vitakavyowaondolea watu wetu mateso haya.”
Sheikh Al-Khatib alihitimisha kwa kusema: “Kinachobaki ni kufanya upya wito wetu kwa mamlaka ya Lebanon ili irejeshe uhusiano na Jamhuri ya Kiislamu katika hali yake ya awali, hususan katika ngazi ya kidiplomasia, pamoja na kurejeshwa safari za moja kwa moja za anga kati ya Beirut na Tehran, kutokana na matatizo wanayokumbana nayo Walebanon na Wairani katika kusafiri kati ya Lebanon na Iran.”
Maoni yako