Jumamosi 12 Septemba 2026 - 22:00
Mtafiti wa Indonesia: Bila ya mazungumzo, umoja hauwezekani

Hawzah/ Naibu Mwenyekiti wa Baraza la Maulamaa wa Indonesia huko Java ya Kati, Profesa Dkt. Haj Abu Hafsin, mwenye shahada ya Uzamili na Udaktari wa Falsafa, amesisitiza kuwa; umoja baina ya madhehebu hauwezekani bila ya mazungumzo.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Naibu Mwenyekiti wa Baraza la Maulamaa wa Indonesia huko Java ya Kati, Profesa Dkt. Haj Abu Hafsin, katika Semina ya Kitaifa ya “Mtazamo wa Kiislamu wa Kati ya Madhehebu” iliyofanyika katika ukumbi wa Astina, Hoteli ya Grasia, Semarang, Jumamosi (5 Septemba 2026), katika hotuba yake huku akisisitiza umoja unaojengwa kwa msingi wa mazungumzo, alieleza wazi kwamba: Mazungumzo ni njia ya kujenga umoja miongoni mwa tofauti.

Mkutano huo pia uliwakutanisha Profesa Sumanto Al-Qurbawi kutoka Chuo Kikuu cha Kikristo cha Satya Wacana (UKSW) Salatiga, Mwenyekiti Mkuu wa Baraza Kuu la Ahlul-Bayt nchini Indonesia, Profesa Zahir Yahya, Profesa Rozihan kutoka Jumuiya ya Wanahabari wa Kiislamu (PWI) ya Muhammadiyah Java ya Kati, pamoja na Mchungaji Ariyanta Nugroho kutoka Kanisa la JAGI. Majadiliano hayo yaliongozwa na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Jukwaa la Kuishi Pamoja Dini za Indonesia, K.H. Dkt. S. Taslim Shihlan.

Katika hotuba yake, Abu Hafsin alirejea mwelekeo wa baadhi ya watu wa kuifanya tafsiri yao ya kidini kuwa ndiyo ya mwisho na isiyoweza kupingwa, na kusema: Pale ambapo tafsiri moja inapoaminiwa kuwa ndiyo ukweli pekee, huku wakati huo huo mtazamo mwingine ukitambuliwa mara moja kuwa ni kosa, nafasi ya kufikia uelewano wa pande zote huzidi kuwa finyu siku baada ya siku.

Aliongeza: Masuala yote ya kidini hayapo katika eneo lenye asili ya kuwa la moja kwa moja na lisilopingika. Baadhi yake ni matokeo ya usomaji na tafsiri ya mwanadamu. Kwa hiyo, tofauti za mitazamo katika kuelewa masuala ya aina hii ni ukweli unaopaswa kuwekwa katika nafasi yake kwa namna inayofaa.

Mtafiti huyo wa masuala ya dini alikumbusha: Tatizo jingine hujitokeza pale ambapo kuishi kwa pamoja kunapoeleweka tu kama jambo linaloweza kuundwa kupitia sheria au kanuni rasmi. Ni kweli kwamba sheria inaweza kudhibiti mwenendo wa mwanadamu katika mazingira ya umma, lakini mahusiano ambayo kwa kweli yana msingi wa kuishi pamoja hayaibuki moja kwa moja kutokana na ulazima wa kutii kanuni fulani. Kwa hiyo, kujenga mahusiano baina ya madhehebu pia kunahitaji mabadiliko katika namna ya kuangalia tofauti. Abu Hafsin alikumbusha kwamba; mahusiano baina ya makundi hayapaswi daima kuwekwa katika mfumo wa siasa na maslahi.

Aliongeza: “Ikiwa mtazamo wetu bado ni mtazamo unaozingatia siasa na maslahi, mazungumzo yatakuwa magumu kutokea.”

Abu Hafsin, huku akisisitiza uwepo wa madhehebu ya Shia katika muundo wa fikra na mikondo ya kidini nchini Indonesia, alieleza wazi kwamba: Kuwa na uwazi kwa kundi ambalo hadi sasa mara nyingi limewekwa nje ya mkondo mkuu, inapaswa kuwa sehemu ya juhudi za kujenga mahusiano yaliyo wazi zaidi.

Alisema: “Ikiwa ningekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Maulamaa wa Indonesia ndani ya Java ya Kati, ningeahidi kuwapokea Shia kama mwanachama wa Baraza la Maulamaa wa Indonesia ndani ya Java ya Kati.”

Mtazamo huu unaonesha misingi ambayo Abu Hafsin alisisitiza katika kujenga mahusiano baina ya madhehebu. Umoja hauhitaji kuondoa tofauti au kulazimisha tafsiri moja ili ikubalike na pande zote, kinachohitajika ni utayari wa kutambua tofauti, kufungua nafasi ya kukutana, na kuweka mazingira kwa ajili ya mazungumzo yatakayowezesha kila upande kuelewana na upande mwingine.

Ni katika mfumo huu ambapo mazungumzo si jambo la ziada tu katika fikra ya umoja, bali ni njia inayowezesha umoja kukua bila kuhitaji kuondolewa kwa tofauti.

Inakumbukwa kwamba semina hii iliwakutanisha viongozi wa Kiislamu, wasomi wa vyuo vikuu na viongozi wa dini kutoka katika misingi mbalimbali, kwa lengo la kujadili mahusiano baina ya madhehebu na umuhimu wa kujenga umoja.

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha