Kwa mujibu wa ripoti ya Kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, kufuatia shambulio la kujitoa muhanga lililolenga Msikiti wa “Khadija al-Kubra (ra)” wa Mashia katika mji wa Islamabad, maelfu ya wakazi wa Kargil, India walifanya maandamano makubwa na ya amani, wakilaani vikali uhalifu huo na kuonesha mshikamano wao na familia za mashahidi; mkusanyiko uliobeba ujumbe wa wazi wa umoja, kupambana na ugaidi na kulinda usalama wa maeneo ya ibada.
Hujjatul-Islam Sheikh Nazir Mahdi Muhammadi, mwanachuoni mashuhuri wa Kargil, India, katika hotuba yake alisisitiza kwamba; mashambulizi kama haya yanaonesha sura halisi na chafu ya ugaidi, na kwamba wahalifu wa vitendo hivyo hawana uhusiano wowote na Uislamu na mafundisho yake ya asili, kwa sababu kuwaua watu wasio na hatia na waumini wanaoabudu ni uhalifu mkubwa dhidi ya ubinadamu na lazima ulaaniwe kwa uthabiti bila masharti yoyote.
Wasiwasi kuhusu kushambuliwa tena Mashia Pakistan
Aliendelea kusema, akirejea kulengwa mara kwa mara kwa Mashia nchini Pakistan, kwamba jambo hilo linatia wasiwasi mkubwa na ni changamoto kubwa katika kiwango cha kimataifa. Alitoa wito kwa jamii ya kimataifa na mashirika ya haki za binadamu kuchukua hatua madhubuti na za vitendo katika kupambana na ugaidi, kulinda jamii ya Mashia na kuhakikisha usalama wa maeneo ya ibada.
Rambirambi kwa familia za mashahidi na kusisitiza umoja
Jumuiya ya Wanazuoni wa Ithna-Ashariyya wa Kargil, pamoja na kutoa rambirambi za dhati kwa familia za mashahidi wa tukio hilo, waliombea majeruhi wapone kikamilifu, na wakasisitiza tena msimamo wao thabiti wa kupambana na ugaidi, vurugu za kimadhehebu na aina yoyote ya misimamo mikali.
Maoni yako