Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Habari la Hawza kutoka Tehran, Mohammad Ali Amani, Katibu Mkuu wa Chama cha Mu’talifah ya Kiislamu, katika barua ya wazi aliyomwandikia Xi Jinping, Katibu Mkuu wa Chama cha Kikomunisti cha China, huku akirejelea mkutano wake ujao na Donald Trump, sambamba na kulaani vikali utendaji wa Rais wa Marekani, ameitaka China kuwasilisha vipaumbele vinne vya msingi katika mkutano huo.
Amani katika barua hiyo amemtaja Trump kuwa ni mhalifu wa kivita na ametangaza kwamba; kwa mtazamo wa taifa la Iran, damu ya Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi ya Kiislamu, makamanda na wanasayansi wa nchi hiyo imo mikononi mwake.
Alisisitiza kuwa: Iran inaona haki ya kufuatilia kisheria na kulipiza kisasi dhidi ya wahusika wa jinai hizi kuwa ni haki isiyokanushika.
Katibu Mkuu wa Chama cha Mu’talifah ya Kiislamu pia alisisitiza umuhimu wa kupokea fidia ya vita kutoka Marekani, kurejeshwa kikamilifu kwa mali za Iran zilizozuiliwa, pamoja na kuthibitishwa kwa usalama wa Mlango wa Hormuz kama sehemu inayotegemea usalama wa taifa wa Iran. Aidha alionya kuwa aina yoyote ya kurejea kwenye sera ya “shinikizo la kiwango cha juu” itakabiliwa na jibu kali.
Katika sehemu nyingine ya barua hiyo, Amani ameitaja China kuwa ni mshirika wa kimkakati, na ameitaka katika mkutano wake na Trump kusimama dhidi ya sera za upande mmoja za Marekani na kutaka kuondolewa kwa vikwazo visivyo vya kisheria.
Mwishoni mwa barua yake, Amani huku akisisitiza azma ya chuma ya taifa la Iran na ushindi wa mwisho wa azma hiyo ya kitaifa, ametaka mamlaka na madai ya taifa la Iran yawasilishwe kwa uwazi kwa upande wa Marekani kupitia Xi Jinping.
Maoni yako